Wednesday, June 26, 2013

SUGU AKAMATWA KWA KUMTUKANA WAZIRI MKUU PINDA

.

MBUNGE wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ''Sugu" (Chadema), alikamatwa na polisi mjini hapa jana na kuhojiwa kwa saa mbili na nusu, akidaiwa kumtukana Waziri Mkuu Mizengo Pinda kupitia mtandao wa jamii wa ‘facebook’. Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime, alisema Sugu alikamatwa saa 8.00 mchana akitokea bungeni na kufikishwa katika Kituo cha Polisi cha kati kwa mahojiano.

Misime alisema polisi waliamua kumkamata mbunge huyo baada ya kugundulika kuandika maneno ya kumtukana Waziri Mkuu juu ya utendaji wake.

Mbunge huyo anadaiwa kumtukana Waziri Mkuu kufuatia kauli yake aliyoitoa hivi karibuni bungeni, katika kipindi cha maswali ya papo kwa papo.

Katika kauli yake hiyo, Pinda alivitaka vyombo vya dola ikiwemo Jeshi la Polisi kutowavumilia watu wanaotishia amani na utulivu hapa nchini.

"Ni kweli tulimkamata Sugu majira ya saa nane mchana na alihojiwa kuhusiana na tuhuma hizo, lakini alidhaminiwa na Tundu Lissu akiwa na mwalimu mmoja wa Sekondari ya Viwandani majira ya saa 10.30 jioni," alisema Misime.

"Hata hivyo mbunge huyo analazimika kufika tena kesho (leo) saa tatu asubuhi, kwa ajili ya kuendelea na mahojiano zaidi kuhusiana na kauli yake katika mtandao huo" alisisitiza Misime.

"Kwa leo (jana), tumekamilisha taratibu zetu ila tutaendelea kwa hatua zaidi kesho (leo), mara atakapofika kwani anatakiwa kufika asubuhi kesho," alisema Misime.

Mkuu huyo wa Jeshi la Polisi mkoani hapa, alisema Polisi itaendelea kumchukulia hatua zaidi kadiri itakavyoona inafaa, ikiwemo kumpeleka katika vyombo vya sheria.

Kamanda alisema Polisi haitasita kumkamata mtu yeyote ambaye ataonyesha kupandikiza mbegu za chuki ambazo zinaweza kuvunja amani na utulivu wa nchi na kuwataka watumiaji wa mitandao hiyo kuitumia kwa minajiri iliyokusudiwa na si kutukana.

Hivi karibuni kumezuka tabia ya baadhi ya wanasiasa kutumia mitandao ya kijamii kuwachafua watu mbalimbali, wakiwemo viongozi wa serikali kwa manufaa yao.

Kauli ambazo zimekuwa zikiandikwa na kuwekwa katika mitandao hiyo, zimekuwa zikijenga chuki kati ya wananchi na serikali yao ikiwemo viongozi.

No comments: