Monday, February 25, 2013

MAUAJI YA PADRI MUSHI WATUHUMIWA TISA (9) WAHOJIWA

.

 Jeshi la Polisi Zanzibar limeanza kuwahoji watu tisa kuhusiana na mauaji ya Padri Evaristus Mushi, wa Kanisa Katoliki Zanzibar, aliyeuawa kwa kupigwa risasi Jumapili iliyopita na watu wasiojulikana.

Padri Mushi alizikwa juzi katika makaburi ya mapadri eneo la Kitope Mkoa Kaskazini Unguja.

Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Zanzibar, Yussuf Ilembo, alisema watu hao walikamatwa na kikosi kazi kilichoundwa kwa kuwahusisha maafisa wa upelelezi kutoka Tanzania Bara na Zanzibar.

“Watu tisa tumewakamata na kuwahoji kama hatua ya kwanza kuwatafuta na kuwakamata watu waliohusika na mauaji, Tumefikia hatua kubwa ya kuwasaka watu hao,” alisema Ilembo.
Hata hivyo, alisema ni mapema kutaja majina na mitaa wanayoishi kutokana na kuhofia kuvuruga uchunguzi na kuongeza kuwa  timu ya wapelelezi inaendelea na kazi yake ikiwamo kukusanya taarifa za kusaidia kuwapata wahalifu hao.

Alisema wananchi wanapaswa kulisaidia Jeshi la Polisi kutoa taarifa za siri kuhusu watu wanaowatilia shaka kuhusiana na vitendo vya hujuma dhidi ya viongozi wa dini.
Kuhusu watu watatu kudaiwa wamekamatwa huko Mombasa, Kenya, Ilembo alisema taarifa hizo hazina ukweli ingawa wanaendelea na uchunguzi kwa kushirikiana na vyombo vya ndani na nje.

MAKACHERO WA NJE KUWASILI
Naye Waziri wa Nchi, Ofisi wa Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud Mohamed, alisema mpango wa kuwaleta makachero wa kimataifa umefikia hatua nzuri na wakati wowote watawasili Zanzibar.

Aboud alisema hatua hiyo ni utekelezaji wa agizo lililotolewa na Rais Jakaya Kikwete na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, kuvitaka vikosi vya ulinzi kushirikiana na kukaribisha vikosi vya nchi rafiki kufanikisha msako huo.

“Tunatafuta shina na mizizi ya uahalifu huu mahali popote ulipo, tuko tayari kumkamata mtu yeyote bila ya kujali wadhifa, cheo au jina lake,” alisema na kuongeza:

“Ndiyo maana tumeamua kukaribisha watu wenye utaalam mkubwa katika masuala ya upelelezi na lengo letui ni kukusanya ushahidi wa kutosha.”

Alisema tayari vikosi vya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar  (SMZ) vimeingia kazini kwa kushirikiana na vya Muungano na Jeshi la Polisi na kuimarisha doria maalum hasa katika maeneo nyeti ya kuingia na kutoka.

Waziri Aboud aliongeza kuwa Rais Shein ameiagiza timu ya upelelezi kumpatia taarifa ya maendeleo kila baada ya muda maalum.

ASKOFU LEBULU ATOA KAULI KALI

Akofu  Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo la Arusha, Josephat Lebulu, amesema, Wakristu wanao uwezo wa kulipiza kisasi dhidi ya mauaji ya viongozi wao yanayofanywa na aliowaita mashetani na mawakala wao na wangekuwa na haki ya kufanya hivyo, lakini, Kristo, anawataka wasilipize kisasi ili kumpa shetani ushindi.

“Sisi siyo wapumbavu na kwamba hatuwezi kufanya chochote…tunavutwa tu na huruma ya Mwenyezi Mungu tukae kimya, lakini hakuna mwanadamu yeyote anayeweza kuvumilia hili. Katika mazingira halisi ya kibinadamu, hakuna hata mmoja ambaye atafurahia mauaji haya isipokuwa shetani na mawakala wake,” alisema.

Askofu huyo aliwataka Wakristu na waumini wa dini nyingine wenye mapenzi mema, wasitawaliwe na hasira, chuki wala mioyo ya kulipa kisasi kwa sababu Yesu Kristu amewataka wasifanye hivyo, ingawa uwezo wa kufanya hivyo wanao na haki ingekuwa upande wao.

Alisema hayo katika mahubiri yake ya Misa ya Wafu ya kumwombea marehemu Padri Mushi.

Katika misa hiyo iliyofanyika katika Kanisa la Mtakatifu Theresa wa Mtoto Yesu jijini hapa jana na kuhudhuriwa na mamia ya waumini wa dini hiyo na wa madhehebu mengine, Askofu Mkuu Lebulu, alisema: “Tusilipe kisasi, bali tushinde kwa yaliyo mema.”

“Kama Mungu yupo nasi na yupo upande wetu, hata kama kwa mabavu na bunduki, hakuna wa kututenganisha na upendo wa Kristu. Je, ni dhiki, njaa, uchi, hatari au upanga,” alihoji na kuongeza: “Lakini haya yote tunayashinda kwa Jina la  Yesu na yeye anatupenda na hakuna chochote kitakachotutenga na upendo wa Kristu.”
Akizungumzia mauaji hayo, alisema wanaamini ukweli wa mambo hayo yatajulikana maana hakuna kinachotendeka kwa siri ambacho hudumu hivyo hivyo bila kujulikana.

Askofu Mkuu Lebulu, alisema Watanzania wanalia kama watoto yatima kwa kukosa baba au wazazi na akaelezea kushangazwa kwake kuhusu kauli za vitisho, matusi na kuleta hofu zilizokuwa zikisambazwa na baadhi ya watu kwa njia za CD, kanda na ujumbe wa simu, huku vyombo vya usalama vikitazama tu, halafu baadaye wanalalamika maadili yameshuka.
“Unashangaa vyombo vya usalama vinaangalia tu, zipo kanda nyingi za matusi na vitisho dhidi ya waumini wa dini nyingine…vipo wapi vyombo vya usalama kama wengine wanauawa namna hii. Mungu awaguse mioyo yao na wabadilike na kumgeukia Mungu.
“Mambo hayo watu wa usalama wamezembea, tangu awali kulikuwapo na viashiria vingi sana vya kuwapo hofu ya mauaji, lakini kwa nini hawashughulikiwi,” alihoji na kuongeza, “pengine hapa kuna siri imejificha.”

Alilaani pia mauaji ya Mchungaji Mathayo Kachila (45), wa Kanisa la Pentekoste la Assemblies of God, mkoani Geita, uchomaji moto wa makanisa na tukio la kumwagiwa tindikali kwa Sheikh huko Zanzibar kunakofanywa na baadhi ya watu kwa malengo wanayoyajua wao wenyewe na akasema vitendo hivyo havisaidii kuleta amani ya taifa.

No comments: